Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amemuagiza Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri
Mkuu (Sera na Bunge), Bw. Uledi Mussa afuatilie malipo ya kiwanja
kilichouzwa na CDA kwa sh. milioni 240 wakati fedha iliyoingia ofisini
ikiwa ni sh. milioni 6 tu.
“Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu, ninataka ufuatilie mauzo ya
kiwanja namba 26 block AA eneo la Kikuyu East ambacho kimeuzwa kwa sh.
milioni 240 lakini fedha iliyoingia CDA ni sh. milioni 6 tu. Nataka
kujua nani ameingiza milioni 6 na nani kachukua hizo sh. milioni 234,”
amesema.
Waziri Mkuu ametoa agizo hilo leo mchana wakati akizungumza na watumishi
na viongozi wa Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu Dodoma (CDA) kwenye
ukumbi wa Hazina ndogo mjini Dodoma.
Bila kutoa ufafanuzi zaidi, Waziri Mkuu amesema eneo hilo lilipaswa kuwa
na kituo cha mafuta na akataka apatiwe taarifa mapema iwezekanavyo.
Pia amemwagiza Katibu Mkuu huyo afuatilie mkataba wa upangishaji wa
jengo la CDA ambalo wamepangishwa taasisi ya Tunakopesha Limited kwa
madai kuwa mhusika alipewa bure na sasa anataka kulipangisha tena ili
apate cha juu.
Waziri Mkuu amewaonya watumishi hao pamoja na viongozi wao waache tabia
ya kushirikiana na madalali kuuza viwanja na akawataka wachape kazi
wakijielekeza na kasi ya Serikali ya kuhamia Dodoma.
“Tabia ya watumishi kushirikiana na madalali kuuza ardhi sasa basi. Hata
hivyo, nimefarijika kukuta mmeanza kuweka mfumo wa kielektoniki katika
baadhi ya huduma. Ni lazima mauzo ya viwanja sasa hivi yafanyike kwa
njia ya kieletroniki, madalali hawana nafasi,” amesisitiza.
Ameutaka uongozi wa CDA uongeze kasi ya upimaji viwanja kwa sababu
mahitaji ni makubwa lakini akaonya kuwa wakati zoezi hilo likifanyika,
wananchi walionunua viwanja na bado hawajamalizia kuvilipia,
wasinyang’anywe kwa kigezo cha kutaka kuwauzia wengine.
“Mimi nataka idadi ya viwanja vilivyopimwa iongezeke. Lakini pia
msitumie fursa hii kuwanyang’anya watu wenye umiliki halali eti kwa
sababu Serikali inataka idadi ya viwanja vilivyopimwa iongezeke,”
amesema.
“Kama mtu amepewa offer au hati yake asinyang’anywe hata kama amelipia
nusu asinyang’anywe. Ahimizwe kumalizia hilo deni na ninyi kazi yenu ni
kupima viwanja vingine,” amesisitiza.
“Natambua mnayo benki ya viwanja, lakini inabidi muongeze idadi ya
viwanja vingi zaidi. Tumeita wawekezaji waje kujenga nyumba za kuishi
watumishi, mahoteli na viwanda na maeneo yote haya inabidi yatengwe
rasmi,” amesema.
Amesema jumla ya viwanja 70,000 vimepimwa tangu CDA ianzishwe mwaka
1973. Amesema kama wataendelea na kasi hiyo wakati mahitaji
yameongezeka, itawachukua zaidi ya miaka 40 kukamilisha mahitaji ya
viwanja 100,000 ambavyo vinatarajiwa kuanza kupimwa hivi karibuni.
Mapema, akitoa taarifa mbele ya Waziri Mkuu, Mkurugenzi Mkuu wa CDA,
Eng. Paskasi Muragili amesema usanifu wa upimaji viwanja 20,000
umekamilika na kwamba wana lengo la kupima viwanja vingine 100,000
ifikapo Juni 2017.
Waziri Mkuu alitembelea Ofisi ya CDA na kukagua mfumo wa utunzaji
mafaili wa zamani pamoja na uhamishaji wa taarifa za wenye viwanja
kwenye mfumo wa kompyuta. Pia alikagua mifumo ya uuzaji viwanja kwa njia
ya mtandao ambayo hata hivyo bado haijakamilika.
0 comments:
Post a Comment