Propela

aa

million ads

Millionaire  Ads

Sunday, March 12, 2017

Wanachama wa Chadema wapigwa, wachaniwa mashati

Dodoma. Mwenyekiti wa Chadema wa Kanda ya Kati, Alphonce Mbasa amesema wanachama wao waliopigwa mjini Dodoma na wafuasi wa CCM, pia wamechaniwa mashati yao.
Akizungumzia tukio la Mbunge wa viti maalumu (Chadema), Kunti Majala kubebwa mzobemzobe kumnusuru asipate kipigo kutoka kwa wafuasi wa chama hicho, Mbasa amesema watu aliokuwa nao mbunge huyo wamepigwa.
“Ni kweli tukio hilo lipo. Waliopigwa zaidi ni dereva Stephen Masawe na mtumishi wa chama wa kanda, Justin Wiliam ambao kwa sasa taratibu zinafanyika ili wapelekwe hospitali. Lakini mbunge aliokolewa na polisi ingawa alisukumwasukumwa,”amesema Mbasa.
Tukio hilo lilitokea saa 7:00 mchana wakati Kunti na wenzake wawili walipopita mbele ya jengo la makao makuu ya CCM, maarufu kama White House ambamo mkutano wa Halmashauri Kuu ya chama hicho ulikuwa ukiendelea. Wakati mkutano ukiendelea, gari la Chadema lilipita karibu mara tatu likiwa linapeperusha bendera za chama hicho cha upinzani kabla ya kusimamishwa baada ya kupita karibu zaidi.
Kipigo hicho kilifuatia gari hilo kusimamishwa na watu waliokuwa wamevalia nguo za kijani ambao walizuia barabarani na hivyo kumlazimu dereva kusimama na ndipo walipoanza kupigwa.
Hata hivyo, Mbasa amesema gari hilo lilikuwa limefungwa bendera kubwa mbili ambazo wakati wote hutumika katika magari hayo yaliyoandikwa “M4C” ubavuni na ndiyo sababu likatambulika kwa haraka kuwa ni la Chadema.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Lazaro Mambosasa amesema hakuwa na taarifa za tukio hilo kwa sababu alikuwa katika msafara wa viongozi na ameahidi kulifuatilia.

0 comments:

Post a Comment