SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF) limefuta adhabu ya kadi nyekundu
aliyooneshwa nahodha wa Simba, Jonas Mkude katika mechi ya timu hiyo
dhidi ya Yanga iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa Dar es Salaam mwishoni
mwa wiki iliyopita.
Kama angekutwa na hatia na kadi hiyo kubaki, Mkude angekosa mechi tatu
na kamati ingemhukumu kifungo cha kuanzia miezi mitatu adhabu ambayo
hupewa mchezaji aliyeoneshwa kadi nyekundu ya moja kwa moja na
kumshambulia mtu ambaye hakuwa na mpira.
Kuondolewa kwa adhabu hiyo kumemwepusha Mkude na kifungo cha kukosa mechi tatu, na adhabu ya kufungiwa si chini ya miezi mitatu.
Hiyo ni kutokana na aina ya kosa hilo kwamba mbali na kufuta kadi hiyo,
kamati ya bodi ya ligi ya uendeshaji na usimamizi wa ligi imewaweka
kiporo waamuzi wawili wa mechi hiyo Martin Saanya (katikati) na Samwel
Mpenzu (pembeni) wakichunguzwa kuhusu uchezeshaji wao wa mechi hiyo.
Mechi hiyo iliyoisha kwa sare ya bao 1-1 ilitawaliwa na vurugu
iliyosababisha kuharibika kwa miundombinu ya Uwanja wa Taifa, ikiwa ni
pamoja na kuvunjwa mageti na kung’olewa viti.
Mwamuzi wa mechi hiyo, Martin Saanya alimwonesha Mkude kadi nyekundu
ikidaiwa kuwa nahodha huyo alimpiga baada ya kukubali bao la kuongoza la
Yanga lililofungwa na Amisi Tambwe ambaye kabla ya kufanya hivyo
alishika mpira na mkono na ndipo kilipozuka kizaazaa.
Lakini taarifa ya TFF kwa vyombo vya habari jana ilisema kamati ya bodi
ya ligi ya uendeshaji na usimamizi wa ligi iliyokutana juzi iliifuta
adhabu hiyo ya Mkude baada ya kuthibitika pasi na shaka kuwa nahodha
huyo hakustahili adhabu hiyo.
“Mbali na ripoti ya kamishna na kupitia tena mkanda wa mechi hiyo
iliyooneshwa ‘live’ kama inaendelea na uchunguzi wa jambo lingine kuhusu
uchezeshaji wa mwamuzi wa mechi hiyo Martin Saanya na wasaidizi wake
Samwel Mpenzu na Ferdinand Chacha kabla ya kutangaza uamuzi wake,”
ilisema taarifa hiyo.
Hata hivyo habari za uhakika zilizopatikana juzi kutoka ndani ya kikao
hicho zilidai kamati iliwafungia miaka miwili Saanya na Mpenzu. Aidha,
kamati hiyo imeipiga faini ya Sh milioni tano klabu ya Simba kwa kitendo
cha mashabiki wake kung’oa viti katika mechi hiyo na kuiagiza ilipe
gharama za uharibifu zilizofanywa siku hiyo.
“Kamati hiyo katika kikao chake imekilaani kitendo hicho na kuionya
klabu hiyo kuwa vitendo vya aina hiyo vikiendelea itakabiliwa na adhabu
kali ikiwemo kucheza bila mashabiki, adhabu hii ya Simba imetolewa kwa
mujibu wa kanuni ya 42(3) na 24(7) za Ligi Kuu,” ilisema taarifa hiyo..
Mwingine aliyepitiwa na ‘rungu’ la adhabu katika mechi hiyo ni Ofisa
habari wa Simba Haji Manara aliyetozwa faini ya Sh 200,000 kwa kitendo
chake cha kuingia uwanjani baada ya mechi hiyo wakati yeye hakuwa
miongoni mwa maofisa wa mechi waliotakiwa kuingia katika eneo hilo.
Aidha, Azam imepigwa faini ya Sh milioni tatu kwa kuvaa nembo ya
mdhamini wa Ligi Kuu mkono mmoja badala ya miwili, jambo ambalo ni
kinyume na kanuni ya 13 (1) na adhabu hiyo imetolewa kwa mujibu wa
kanuni ya 13 (6).
Nayo JKT Ruvu imepewa onyo na kutozwa faini ya Sh 500,000 baada ya
msimamizi wa kituo na ofisa wa bodi ya ligi kushambuliwa na mashabiki wa
timu hiyo katika mechi dhidi ya Mbeya City kwenye uwanja wa Mabatini
Mlandizi, Pwani.
Shabiki huyo amefungiwa miezi 12 na iwapo vitendo hivyo vitaendelea uwanja huo utafungiwa kutumika kwa mechi za Ligi Kuu.
Aidha Mwamuzi Ahmed Seif amefungiwa miezi sita kwa kushindwa kumudu
mechi ya African Lyon dhidi ya Mbao FC, ikiwemo kutoa penalti
isiyostahili. Mwamuzi huyo pia alipata alama za chini ambazo
hazikumruhusu kucheza Ligi Kuu.
“Pia makamisaa David Lugenge na Godbless Kimaro wamepewa onyo kwa
kuwasilisha taarifa zenye upungufu katika mechi za raundi ya tano na
saba walizozisimamia,” ilisomeka taraifa hiyo.
0 comments:
Post a Comment